More about me...

My photo
Kilifi, Coast, Kenya
Informing is not only my profession but also passion

Welcome

Welcome

Tuesday, 26 August 2014

Watangazaji wafunzwe Kiswahili zaidi


Mojawapo ya vigezo vinavyozingatiwa wakati wa usajili wa wanafunzi katika taaluma za uanahabari ni ukwasi wa lugha. Taasisi nyingi nchini Kenya zinazotoa mafunzo hayo katika viwango mbali mbali vikiwemo shahada, diploma na vyeti hususani katika utangazaji hupendelea wanafunzi waliofanya vizuri katika somo la Kiingereza, Kiswahili au yote mawili.

Sababu ya kufanya hivyo ni kuhakikisha wanafunzi hao ambao ni wataalamu wa badaye wana uwezo wa kujieleza kwa lugha yoyote kati ya hizo mbili za kitaifa iwe ni kwenye magazeti, majarida, redio, runinga au hata mtandaoni. Jukumu kubwa zaidi la mwanahabari ni kuwasilisha ujumbe kwa hadhira na ni dhahiri kwamba ala muhimu anayohitaji kufanyia hivyo ni lugha.

Hapo awali, kulingana na katiba, lugha ya Kiingereza ilitambulika kama lugha ya kitaifa ilhali ile ya Kiswahili ikasemekana kuwa ni lugha rasmi. Hata hivyo, kulingana na katiba mpya iliyoidhinishwa kupitia kura ya maoni ya mwaka wa 2010, Kiswahili pia kinatambulika kama lugha ya kitaifa na inachukuliwa kwa usawa na Kiingereza.

Cha kushangaza ni kwamba lugha ya Kiswahili haijatiliwa mkazo katika kuwafunza wanaodhamiria kuwa watangazaji katika baadhi ya vyuo vikuu na vyuo anuai. Mfano mzuri ni chuo kikuu cha Moi, kinachotoa mafunzo tofauti tofauti yanayohusiana na utangazaji. Katika kitivo cha sayansi za habari, kunayo taaluma ya sayansi ya uanahabari. Kati ya jumla ya masomo 56 anayofaa kuyapitia mwanafunzi kabla ahitimu, mawili tu ndiyo hufunzwa kwa lugha ya Kiswahili.

Hali hii imesababisha wanafunzi wengi kutoimarika katika kuandika au kuzungumza kwa lugha ya Kiswahili, jambo ambalo huathiri utendakazi wao hasa wale wanaoajiriwa katika vyumba vya habari vinavyotangaza au kuandika kwa Kiswahili. Wanapolazimika kuitumia lugha hiyo, hufanya hivyo wakiwa na mtazamo hasi au bila kuzingatia usahihi wa kisarufi. Wanahabari hao mara nyingi hushindwa na tafsiri za maneno ya kimsingi hivyo basi hutumia njia ya mkato ya kutohoa misamiati mingi kutoka kwa lugha zengine.

Kuna haja ya taasisi mbali mbali kufanya mageuzi katika mtaala wao, si katika taaluza za utangazaji tu bali na nyenginezo pia. Mtu anayesomea kozi ya kibiashara kwa mfano, anayeazimia kufanya kazi kama mkurugenzi wa kampuni, ni muhimu ajue kuwasiliana kwa lugha ya Kiswahili kando na ya Kiingereza, na si Kiswahili tu bali Kiswahili sanifu.

No comments:

Post a Comment