More about me...

My photo
Kilifi, Coast, Kenya
Informing is not only my profession but also passion

Welcome

Welcome

Monday, 18 August 2014

Dondoo za spoti- 15/8/2014



Gor Mahia yaaga mashindano
Klabu ya Gor Mahia iliyowakilisha Kenya katika michuano ya CECAFA Kagame Cup nchini Rwanda ilibanduliwa mapema baada ya kulazimishwa sare ya mabao 2-2 na APR siku ya Jumamosi. Gor ilihitajika kushinda mechi hiyo ili kufufua matumaini ya kusalia katika mashindano hayo baada ya kupoteza mechi mbili za kwanza katika hatua ya makundi.

Gor Mahia ilicheza mechi yake ya mwisho jana jioni dhidi ya Telecom ya Djibout, mechi ambayo matokeo yake hayangeathiri popote kwani timu zote mbili tayari zilikuwa zimepoteza nafasi ya kufuzu kwa hatua ya muondoano.

Gor ilifedheheka kwa kushika mkia katika kundi B baada ya kuvuna alama mbili tu ndani ya mechi nne. Inatarajiwa kurejea nyumbani hii leo ili iendeleze kibarua cha kutetea taji ya ligi kuu ya Premier nchini, dhidi ya SoNy Sugar siku ya Jumapili.

Manchester United yaanza kwa kichapo
Vigogo wa Wingereza Manchester United walianza msimu mpya wa ligi kuu ya Premier nchini humo kwa mshangao baada ya kuchapwa mabao 2-1 na Swansea City uwanjani kwao Old Trafford siku ya Jumamosi.

Chini ya mkufunzi mpya Louis van Gaal, United waliingia uwanjani wakiwa na matumaini makubwa hasa baada ya kushinda mechi zao zote sita za matayarisho ya msimu dhidi ya La Galaxy, AS Roma, Inter Milan, Real Madrid, Liverpool na Valencia katika usanjari huo.

Hata hivyo dau lilianza kwenda mrama wakati raia wa Korea Sung-Yueng Ki alipoiweka Swansea kifua mbele mnamo dakika ya 28 ya mchezo. Muda mfupi baada ya mapumziko, nahodha mpya wa Mancheter United Wayne Rooney alisawazishwa kwa bao la mtindo wa pindu kabla Gylfi Sigurdsson kuipa Swansea bao la ushindi, dakika 18 kabla mechi kutamatika. Hiyo ilikuwa mara ya kwanza United kupoteza mechi ya ufunguzi wa msimu wakiwa nyumbani tangu mwaka wa 1972.

Kwa upande wao Arsenal waliponyoka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Crystal Palace nyumbani kwao Emirates, kwa hisani ya mabao ya Laurent Koscielny na Aaron Ramsey waliyoyafunga katika muda wa ziada wa kipindi cha kwanza na cha pili mtawalia.

Kwengineko chipukizi wa Wingereza Raheem Sterling na Daniel Sturridge walisaidia Liverpool kuandikisha ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Southampton jana jioni, kabla Manchester City kuilaza Newcastle kwa mabao 2-0 kupitia mickwaju ya David Silva na Sergio Aguero.

Hivi leo Chelsea watakuwa ugenini dhidi ya timu iliyopandishwa daraja msimu-jana Burnley katika mechi iliyoratibiwa kuanza saa nne kamili usiku.

Je, wajua?
Toni Kroos ameshinda makombe 4 katika mechi 10 za mwisho alizoshiriki!
Tarehe
Kombe
Timu
11/5/2014
Bundesliga
Bayern
17/5/2014
DFB Pokal
Bayern (dhidi ya Borussia Dortmund)
13/7/2014
Kombe la dunia
Ujerumani (dhidi ya Argentina)
12/8/2014
UEFA Super Cup
Real Madrid (dhidi ya Sevilla)