More about me...

My photo
Kilifi, Coast, Kenya
Informing is not only my profession but also passion

Welcome

Welcome

Thursday, 28 June 2012

Fursa niliyoikosa


Je, uliposajiliwa kama mwanafunzi katika bewa kuu la chuo kikuu cha Moi, ilikuwa mara yako ya ngapi kukanyaga ardhi ya mahala hapa? Swali hili, katu haliwezi kuzalisha majibu sawa kwa wadau tofauti tofauti katika taasisi hii ya elimu.
 Kunao waliowahi kuzuru mahali hapa hata kabla hawajajua kwamba huenda hatimaye wakajipata papa hapa katika safari yao ya kutafuta shahada.
Aidha kuna wale ambao, mimi nikiwa mmoja wao, waliyaona mandthari ya Moi mara ya mosi katika pilkapilka za kusajiliwa kiuanagenzi.
Kwa wanafunzi wa shule ya upili ua St. Teresa’s Opanga - iliyoko eneo la Kadongo katika mkoa wa Nyanza, hii leo imekuwa siku njema kwa baadhi yao waliopata nafasi ya kuzuru chuo hiki. Kwa hakika hii ni hatua kabambe sana, hasa tukizingatia saikolojia ya mwanadamu – ambaye hupata mvuto wa kukienzi kitu anachokiona kwa macho kuwa kizuri. Natumai kunao wengine ambao tayari wamepata motisha utakaowatia ngoa na kuwapa msukumo wa kufanya vyema katika mtihani wao wa kitaifa wa KCSE, ili mwisho wa siku nao wajivunie kuwa wana-Moi au chuo kikuu chochote chenginecho.
Wanafunzi wa Teresa's - Chuoni Moi
Dhana ya kwamba wanafunzi hao wamependezewa na mahali hapa ungeithibitisha tu, kama ungepita karibu nao na kutazama tabasamu lililokuwa limetanda nyusoni mwa wengi wao – kama si wote. Wengine hawakutaka kuondoka kisha waisahau siku hii maishani mwao, hivyo basi wakaamua kupiga picha katika maeneo fulani fulani yaliyoonekana kuwavutia zaidi. Wanafunzi hao wametembezwa sehemu mbali mbali zikiwemo ukumbi wa wanafunzi, maktaba, kitivo cha rasilimali-watu, afisi za utawala na kadhalika.
Lakini kwa kauli yangu, wanafunzi hao wameikosa fursa ya dhahabu, ambayo ingewapa taswira kamili ya maisha chuoni humu, kwa kutopelekwa sehemu nyeti kama vile hosteli H na J. Huko, wangejionea maajabu ya mwaka na hata pengine kuchanganyikiwa kwa taarifa-kinzani. Huku muelekezi wao akisema, “Hapa ni H, hosteli inayoishi wanafunzi wa kiume tu…” wakati huo huo anatokezea binti mmoja au wawili wakitoka kuoga na wanaingia ‘vyumbani mwao’. Huko J pia, muelekezi angesema, “Humu ni mwa wasichana sasa…” mara ghafla wanakutana na barobaro limeshikilia kifuko cha ngumuu na linafungua mlango wa ‘chumba chake’!
Hata hivyo, waliyoyapata yanatosha, kwani wanafunzi hao wamejifunza mengi kwa kujionea, kujisomea na hata kwa kusikia pia; hayo yote ni katika fursa waliyopewa, fursa ya kutamanika – Fursa niliyoikosa!!!

No comments:

Post a Comment