More about me...

My photo
Kilifi, Coast, Kenya
Informing is not only my profession but also passion

Welcome

Welcome

Thursday, 4 December 2014

Wanafunzi wazua ghasia na kupora mali chuoni

Kulishuhudiwa maanamano hapo jana katika chuo Kikuu cha Moi, baada ya wanafunzi kugadhabishwa na ukosefu wa nguvu za umeme hasa katika sehemu ya malazi ya SOWETO. Yalianza mwendo wa saa saba mchana na kuendelea kwa zaidi ya masaa matatu.


Wanafunzi hao walibeba matawi huku wakiimba wimbo wa mapambano na kufululiza hadi katika afisi za usimamizi wa chuo ili kueleza kutoridhika kwao. Walitaka kuhutubiwa na Naibu wa Chansela Bw. Richard Mibey, lakini badala yake akawatuma wasaidizi wake wawili kuwatuliza waandamanaji kwa kuwahakikishia kwamba tatizo hilo sugu lingetatuliwa mara moja.

Haikuwa kazi rahisi kwa wawili hao kuzima ghasia hizo hadi mwishowe wakawasiliana na mkurugenzi wa kampuni ya Kenya Power tawi la Eldoret ili afike chuoni humo mara moja. Alipowalisi, mkurugenzi huyo, ambaye alikosa hata nafasi ya kujitambulisha kwa jina, alilazimika kuvumilia matusi na kelele kutoka kwa wanafunzi waliojawa na hasira, kabla hatimaye kutoa hotuba yake kwa kifupi.

“Tayari chuo chenu kimelipa pesa kwa kampuni ya Kenya Power, kwa hivyo kesho asubuhi wafanyikazi wetu watakuwa hapa ili kutatua tatizo hili. Tutaweka mashini mpya ya kudhibiti na kusambaza umeme, shughuli itakayotuchukua siku moja au mbili kuanzia kesho.”

Hotuba hiyo ilisaidia pakubwa katika kutuliza ghasia hizo na hali ya utulivu ikarudi tena chuoni humo, na shughuli nyenginezo zikandelea.

Hata hivyo, mwendo wa saa moja jioni, ghasia hizo zilizuka upya baada ya umeme kutoweka tena na hapo ndipo wanabiashara walihesabu hasara.

Kwa kisingizio cha njaa, wanafunzi hao walivamia soko la mboga na matunda na kuanza kupora chochote chenye ladha ya chakula. Sukuma, kabeji, nyanya, vitunguu, ndizi, parachichi, na kadhalika, wanafunzi walijishindia. Hata vibanda vya soko hilo pia vilikiona cha mtema kuni kwani viligeuzwa maghofu kwa muda usiozidi nusu saa.

Duka la kuuzia vibanzi, chapi na mahamri lililo karibu pia halikusamehewa, kwani pia lilisaidia kukata njaa ya waandamanaji hao. Baadaye walivamia duka lengine mita kadhaa kutoka hapo na kupora chochote kilichokuwa ndani baada ya kufanikiwa kuvunja milango na madirisha.

Hii leo mwendo wa saa tatu gari la kampuni ya Kenya Power limewasili chuoni pamoja na wahandisi na vifaa vyao ili kuanza shughuli ya kurekebisha hitilafu za umeme kwa lengo la kuzuia ghasia kama hizo kutokea tena siku za usoni.

No comments:

Post a Comment