More about me...

My photo
Kilifi, Coast, Kenya
Informing is not only my profession but also passion

Welcome

Welcome

Monday, 28 July 2014

Msalaba Mwekundu Kuimarisha Mazingira



Chama cha Msalaba Mwekundu cha wanafunzi wa chuo kikuu cha Moi, hapo juzi Jumamosi tarehe 26 mwezi Julai kilizindua rasmi mpango wa kuyarembesha mazingira.

Baadhi ya wanachama wakipanda miche
Shughuli hiyo iliyong'oa nanga mwendo wa saa nne asubuhi, ilihusisha upandaji miti katika maeneo mbali mbali ya bewa kuu. Aidha wafuasi waliitumia fursa hiyo kuutambulisha umma kuhusu uwepo wa chama hicho katika taasisi hii.

Moja wapo ya mikakati waliyoitumia ni kuandaa msafara ulioanzia nje ya jumba la ukumbi wa wanafunzi, chini ya uongozi wa mwenyekiti wa chama hicho Bw. Chris Kimanga. Msafara huo uliojumlisha zaidi ya wanachama hamsini, wakiwa wamebeba bango la chama, ulisonga hadi kituo cha magari kwa mwendo usiokuwa wa kasi, kabla ya kupiga kona kuelekea Magharibi hadi kituo cha ukuzaji miche, maarufu kama ‘Moi University Nursery’, karibu na soko la wazi la ‘Mabbs’.

Ni katika kituo hicho ambapo miche zaidi ya 500 ilipatikana, pamoja na majembe ya kupandia. Kulingana na Bw. David Mitei ambaye ni mmoja wa wasimamizi wa kituo hicho, jamii jirani imekuwa ikinufaika pakubwa na shughuli za kituo hicho. Kwa mfano, taasisi mbali mbali za karibu (kama vile shule na makanisa) zimekuwa zikiwahi miche bila malipo, hii yote ikiwa ni juhudi ya kuyaimarisha mazingira.

Kutoka hapo wanachama wa Msalaba Mwekundu walielekea hadi maeneo ya Hosteli L, ambapo walianza kwa kuipanda miti hiyo ili kujaliza mapengo yaliyoachwa baada ya baadhi ya miti iliyopandwa awali kunyauka au kutonawiri ipasavyo. Baadaye walitapakaa kwengineko, kulikoonekana na uhitaji wa miti, zikiwemo laini za kando ya kibarabara kinachounganisha eneo hilo na Hosteli za Soweto.

Iliyodhaniwa kuwa kazi rahisi ilipevuka upesi na kuwa ngumu na ya kuchokesha, kwani wanachama hao walilazimika kufanya kazi kwenye miale ya jua; kunyosha kamba, kupima hatua sita sita huku wakiweka alama, kuchimba mashimo, kuzika miche na kufunika. Ni shughuli iliyohitaji ushirika, bidii na uvumilivu kwa zaidi ya masaa matatu mfululizo kabla ya kufikia tamati mwendo wa saa nane mchana.

Hatimaye uliwadia ule wakati wa kurudisha nguvu mwilini, ambapo idadi ya wanachama iliongezeka ghafla hadi zaidi ya sabini. Walishirikiana katika riziki nyepesi iliyojumlisha soda ndogo, thuluthi ya mkate wa boflu na pipi mbili kila mmoja kabla ya kufumukana.