More about me...

My photo
Kilifi, Coast, Kenya
Informing is not only my profession but also passion

Welcome

Welcome

Thursday, 22 August 2013

Naisubiri Siku Hiyo



Iwapo kuna siku ya hivi karibuni ninayoingojea kwa hamu na ghamu katika chuo hiki, si nyengine bali ni tarehe sita mwezi ujao wa Septemba.  Tukio ambalo ninalitarajia kwa matamanio makubwa, linaloufanya moyo wangu ukose subira, ni lile la uchaguzi.

Siku hiyo kulingana na ninavyoitabiria, itakuwa muhimu na iliyosheheni shughuli chungu nzima. Nikiwa miongoni mwa maelfu ya wanagenzi wa chuo hiki cha Moi bewa kuu, nitaahirisha shughuli zote ambazo ningepania kuzitekeleza siku hiyo hata kama ni kwa muda tu, ili kuitumia fursa hiyo kuwachagua viongozi wapya watakaoshikilia nafasi mbali mbali katika uongozi wa muungano wa wanafunzi.

Sababu kadhaa zinanishawishi na kuifanya shughuli hiyo ya uchaguzi kuwa yenye umuhimu mkubwa katika maisha yangu kama mwanafunzi wa chuo hiki. Kwanza ni haki ya kidemokrasia. Ikiwa kilio changu cha chini kwa chini kila uchao, cha kutaka haki nyenginezo za msingi kama vile maisha bora kitaendelea kugonga mgongo wa kobe, basi hii nina uhakika wa kuifurahia kwani ni haki isiyohitaji kilio kuipata. Hakuna ajuaye, pengine nitakayemchagua siku hiyo ndiye mkombozi aliyetabiriwa na Yohana mbatizaji na manabii wa kale kwamba atakuja kuniondolea masaibu ya muda.

Pili ni kwamba ninahitaji kutawalwa na kiongozi ninayemuenzi, niliyemkabidhi mamlaka mwenyewe kupitia kura yangu. Iwapo nitaamua kulipa kisogo zoezi la uchaguzi, uamuzi huo usio wa busara hautakuwa na manufaa yoyote kwangu, ila utafananishwa na kujitemea mate usoni mwangu mwenyewe. Nishiriki au nisishiriki, viongozi sharti watachaguliwa na kuanza kazi mara moja. Hapo ndipo nitakapojigundua kumbe mimi ni mtu ‘hivi hivi’, jambo ambalo siku zote nitaishi kujutia hasa viongozi hao watakapoanza kwenda fyongo na kutoyashughulikia maslahi yangu kikamilifu, kinyume na matarajio yangu. Hata ikiwa watafanya vizuri, pia sitakuwa na chochote cha kujivunia kwa ajili yao, nikizingatia kwamba sikuhusika kivyovyote katika kuwachagua.

Kwa mantiki hiyo basi siwezi kamwe kukosa kuivaa mzima mzima shughuli hiyo ijayo ya kukata na shoka. Ikiwa sababu zote hizo hazitoshi, naweka nadhiri ya kuziongeza wakati mwengine. Cha msingi ni kwamba naisubiri siku hiyo kama nilivyoisubiri ile ya tarehe nne mwezi Machi mwaka huu. Swala la iwapo zoezi zima litaendeshwa kwa njia ya kielektroniki au la; kwa foleni au kupitia mtandao; kwa muda mrefu au mfupi; hayo si majukumu yangu. Nina imani na maafisa wa tume huru ya uchaguzi wanaotazamiwa kutajwa hivi karibuni kwamba watalivalia njuga swala zima na kuandaa uchaguzi wa aina yake. Ninachoomba mimi ni uchaguzi uwe wa haki na uwazi jinsi ule wa uraisi ulivyodaiwa kuwa.

Kwa sasa nimeamua kutia masikio nta na kuzifanya zipite juu ya hewa, tetesi kwamba mikutano ya kikabila imeanza kushuhudiwa yenye malengo ya kusimamisha wagombea kwa misingi ya kikabila. Ninachofahamu fika ni kwamba kiongozi yeyote atakayechaguliwa lazima atatoka katika kabila fulani lolote lile. Hivyo basi, nimejifunza tangu utotoni kutojisumbua na wasiwasi wa aina yoyote wa kikabila, kijinsia au kimaeneo kwani binadamu wote ni sawa mbele za Mungu na yeyote anaweza kutunukiwa zawadi ya uongozi. Isitoshe, ninaotaka ni uongozi bora na utapatikana tu ikiwa viongozi watakuwa bora. Je, si wale wa kabila fulani ndio wanaojua ni mtu yupi wao aliye bora?

Hatimaye ninaelekeza dua kwa mwengezi Mungu azidi kunineemesha neema ndogo-ndogo na neema kubwa-kubwa, niweze kuendelea kupumua kwa pumzi yake mwenyewe hadi siku hiyo ya tarehe sita. Pia nawaombea baraka viongozi wote wanaoondoka mamlakani na kheri njema maishani mwao pindi watakapostaafu rasmi. Waendeleze talanta zao za uongozi walizoonyesha wakiwa madarakani kwa muda huo mrefu mno kulingana na katiba ya uongozi. Lakini zaidi ya yote mie nitazidi kushikilia tisti msimamo wangu wa kuisubiri siku hiyo!